| Chapter 1 |
1 |
Habari Njema ya Yesu Kristo, Mwana wa Mungu.*fa* |
2 |
Ilianza kama ilivyoandikwa katika kitabu cha nabii Isaya: "Tazama, namtuma mjumbe wangu akutangulie; yeye atakutayarishia njia yako. |
3 |
Sauti ya mtu imesikika jangwani: `Mtayarishieni Bwana njia yake, nyoosheni mapito yake."` |
4 |
Yohane Mbatizaji alitokea jangwani, akahubiri kwamba ni lazima watu watubu na kubatizwa ili Mungu awasamehe dhambi zao. |
5 |
Watu kutoka sehemu zote za Yudea na wenyeji wote wa Yerusalemu walimwendea, wakaziungama dhambi zao, naye akawabatiza katika mto Yordani. |
6 |
Yohane alikuwa amevaa vazi lililofumwa kwa manyoya ya ngamia, na mkanda wa ngozi kiunoni mwake. Chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwituni. |
7 |
Naye alihubiri akisema, "Baada yangu anakuja mwenye uwezo zaidi kuliko mimi, ambaye mimi sistahili hata kuinama na kufungua kamba za viatu vyake. |
8 |
Mimi ninawabatiza kwa maji, lakini yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu." |
9 |
Siku hizo, Yesu alifika kutoka Nazareti, mji wa Galilaya, akabatizwa na Yohane katika mto Yordani. |
10 |
Mara tu alipotoka majini, aliona mbingu zimefunguliwa, na Roho akishuka juu yake kama njiwa. |
11 |
Sauti ikasikika kutoka mbinguni: "Wewe ni Mwanangu mpendwa, nimependezwa nawe." |
12 |
Mara akaongozwa na Roho kwenda jangwani, |
13 |
akakaa huko siku arubaini akijaribiwa na Shetani. Alikuwa huko pamoja na wanyama wa porini, nao malaika wakawa wanamtumikia. |
14 |
Yohane alipokwisha fungwa gerezani, Yesu alikwenda Galilaya, akahubiri Habari Njema ya Mungu, akisema, |
15 |
"Wakati umetimia, na Ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni na kuiamini Habari Njema!" |
16 |
Alipokuwa anapita kando ya ziwa Galilaya, aliwaona wavuvi wawili: Simoni na Andrea ndugu yake wakivua samaki kwa wavu. |
17 |
Yesu akawaambia, "Nifuateni nami nitawafanya ninyi wavuvi wa watu." |
18 |
Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata. |
19 |
Alipokwenda mbele kidogo, aliwaona Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo. Nao pia walikuwa ndani ya mashua yao wakizitengeneza nyavu zao. |
20 |
Yesu akawaita mara, nao wakamwacha baba yao Zebedayo katika mashua pamoja na wafanyakazi, wakamfuata. |
21 |
Wakafika mjini Kafarnaumu, na mara ilipofika Sabato, Yesu akaingia katika Sunagogi, akaanza kufundisha. |
22 |
Watu wote waliomsikia walishangazwa na mafundisho yake, maana hakuwa anafundisha kama walimu wao wa Sheria, bali kama mtu mwenye mamlaka. |
23 |
Mara akatokea mle ndani ya sunagogi mtu mmoja mwenye pepo mchafu, |
24 |
akapaaza sauti, "Una nini nasi, wewe Yesu wa Nazareti? Je, umekuja kutuangamiza? Najua wewe ni nani: wewe ni Mtakatifu wa Mungu!" |
25 |
Yesu akamkemea, "Nyamaza! Mtoke mtu huyu." |
26 |
Basi, huyo pepo mchafu akamtikisatikisa mtu huyo, kisha akalia kwa sauti kubwa, akamtoka. |
27 |
Watu wote wakashangaa, wakaulizana, "Ni mambo gani haya? Je, ni mafundisho mapya? Mtu huyu anayo mamlaka ya kuamuru hata pepo wachafu, nao wanamtii!" |
28 |
Habari za Yesu zikaenea upesi kila mahali katika wilaya ya Galilaya. |
29 |
Wakatoka katika sunagogi, wakaenda moja kwa moja hadi nyumbani kwa Simoni na Andrea; Yakobo na Yohane walikwenda pamoja nao. |
30 |
Basi, mama mmoja, mkwewe Simoni, alikuwa kitandani ana homa kali. Wakamwarifu Yesu mara alipowasili. |
31 |
Yesu akamwendea huyo mama, akamshika mkono, akamwinua. Na ile homa ikamwacha, akaanza kuwatumikia. |
32 |
Jioni, jua lilipokwisha tua, wakamletea Yesu wagonjwa wote na watu waliopagawa na pepo. |
33 |
Watu wote wa mji ule wakakusanyika nje ya mlango. |
34 |
Naye Yesu akawaponya watu wengi waliokuwa na magonjwa mbalimbali; aliwafukuza pepo wengi, lakini hakuwaruhusu kusema kitu maana walikuwa wanamjua yeye ni nani. |
35 |
Kesho yake, kabla ya mapambazuko, Yesu alitoka, akaenda mahali pa faragha kusali. |
36 |
Simoni na wenzake wakaenda kumtafuta. |
37 |
Walipomwona wakamwambia, "Kila mtu anakutafuta." |
38 |
Yesu akawaambia, "Twendeni katika miji mingine ya jirani nikahubiri huko pia, maana nimekuja kwa sababu hiyo." |
39 |
Basi, akaenda kila mahali Galilaya akihubiri katika masunagogi na kufukuza pepo. |
40 |
Mtu mmoja mwenye ukoma alimwendea Yesu, akapiga magoti, akamwomba, "Ukitaka, waweza kunitakasa!" |
41 |
Yesu akamwonea huruma, akanyosha mkono wake, akamgusa na kumwambia, "Nataka, takasika!" |
42 |
Mara ukoma ukamwacha mtu huyo, akatakasika. |
43 |
Kisha Yesu akamwambia aende zake upesi na kumwonya vikali, |
44 |
"Usimwambie mtu yeyote jambo hili, ila nenda ukajionyeshe kwa kuhani; kisha utoe sadaka kwa ajili ya kutakasika kwako kama alivyoamuru Mose, iwe uthibitisho kwao kwamba umepona." |
45 |
Lakini huyo mtu akaenda, akaanza kueneza habari hiyo kila mahali na kusema mambo mengi hata Yesu hakuweza tena kuingia katika mji wowote waziwazi; ikamlazimu kukaa nje, mahali pa faragha. Hata hivyo, watu wakamwendea kutoka kila upande. |